Usiyaone matatizo ya kiuchumi kama Kikwazo – Mwl Mwakasege

mwakasege

Shalom,

Tunajua unataka uwe na uchumi mzuri. Hii ni kwa mwanadamu yeyote bila kujali mahali alipo,awe anafanya kazi au hata kama hafanyi kazi.

Kuanzia leo na siku kadhaa zitakazofuata,tutajitahidi kukushirikisha misingi kadhaa iliyomo katika biblia,ambayo tunaamini itakusaidia uwe na uchumi mzuri. Msingi wa kwanza ni huu:Badilika unavyoamini juu ya uchumi,utabadilika unvyosema juu ya uchumi,na hali yako ya uchumi itabadilika vivyo hivyo.

Tunaamini ya kuwa; mtu akibadilika anavyoamini atabadilika pia anavyosema;na hali yake ya maisha itabadilika vivyo hivyo.
Jambo hili tunalipata tunaposoma kitabu cha Mithali 23:7 ya kuwa; “Maana aonavyo nafsini mwake,ndivyo alivyo.”
Tafsiri nyingine ya mstari huu inasema;”maana awazavyo nafsini mwake ndivyo alivyo.” Tasfiri nyingine ya mstari huu inasema;”maana aaminivyo nafsini mwake,ndivyo alivyo.” Mstari huu unataka tujue ya kuwa maisha ya mtu alivyo ni matokeo ya awazavyo au aaminivyo au afikirivyo(mindset), nafsini mwake.

Ulivyo kimaisha kwa nje ni matokeo ya msimamo wako wa kimawazo ndani yako. Kwa ulivyo kiuchumi,ni matokeo ya msimamo wako kimawazo(mindset),ulionao ndani yako juu ya uchumi.

Wapelelezi 10 walileta habari mbaya walipotoka kuipeleleza Kaanani,kwa vile waliamini mioyoni mwao ya kuwa “majitu” waliyoyakuta Kaanani yalikuwa kikwazo na pingamizi kwao.Wapelelezi wawili (Yoshua na Kalebu),waliona hayo “majitu” pia lakini mioyoni mwao waliamini tofauti. hawakuyaona majitu kama kikwazo bali waliyaona kama fursa kwao ya kutatua tatizo hilo ili waweze kula.

Soma habari hii katika kitabu cha hesabu 13:32,33 na Hesabu 14:9,28
Matokeo ya tofauti hizo kuwaza na kuamini,kuliamua hatma ya baadaye ya uchumi na maisha yao.Wapelelezi 10 waliishia kulalamika na kushindwa kwenda Kaanani. Na wale wawili (Yoshua na Kalebu) waliweza kwenda Kaanani na wakawa na maisha mazuri.

Wazo tunalokufikirisha siku hii ya leo ni kwamba;Usiyaone matatizo ya kiuchumi yanayokuzunguka kama kikwazo,bali yaone fursa ya kuyatatua ili iwe njia mojawapo ya kuongeza kipato chako. Kumbuka wanaolalamika wanapoona matatizo,wanajipofusha fikra szao wasiona fursa za kimaendeleo katika matatizo hayo.

Mungu awabariki.

Christopher & Diana Mwakasege(Mana Ministry)

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More